TAKUKURU YAWATAKA WATUMISHI KUZINGATIA MAADILI, WANANCHI WAHIMIZWA KUTOA TAARIFA ZA RUSHWA
Taasisi ya
Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoa wa Shinyanga imezitaka taasisi za
umma kutoa huduma kwa kuzingatia misingi ya maadili na uwajibikaji, hatua
ambayo itasaidia kudhibiti vitendo vya rushwa.
Akitoa
taarifa ya utendaji kwa kipindi cha robo mwaka kuanzia Oktoba hadi Desemba
2025, Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Shinyanga, Donacian Kessy, amesema kuzingatia
maadili ni msingi muhimu wa kukomesha vitendo vya rushwa na kuboresha utoaji wa
huduma.
Amesema
katika kipindi hicho, TAKUKURU imefuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo
yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 3 na kufanikiwa kuokoa vifaa vya
ujenzi vyenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 50, ikiwemo nondo, vigae, vifaa
vya umeme na maji ambavyo havikuwasilishwa na mzabuni kwenye mradi wa ujenzi wa nyumba ya mtumishi katika Shule ya Msingi Magongwa Halmashauri ya Msalala wilayani Kahama.
Kwa upande
wa ukusanyaji mapato, taasisi hiyo imeimarisha udhibiti wa ukwepaji ushuru wa
mazao katika Manispaa ya Shinyanga kupitia ufuatiliaji wa mifumo na doria
maalum. Aidha, baada ya kutoa elimu ya maadili kwa watumishi wa afya wa
Halmashauri ya Ushetu kufuatia malalamiko ya wananchi, mapato ya idara ya afya yameongezeka
kutoka shilingi milioni 3 hadi milioni 14 kwa mwezi huku huduma zikiboreshwa.
Katika
kipindi hicho, TAKUKURU imepokea malalamiko 39, yakiwemo 22 yanayohusu rushwa, ambapo
kati ya kesi 4 zilizofunguliwa Mahakamani moja imetolewa uamuzi na Jamhuri imeshinda kesi hiyo.
Kessy amewahimiza wananchi kuendelea
kushirikiana na TAKUKURU kwa kutoa taarifa za viashiria vya rushwa kupitia
namba ya simu ya bure.









Post a Comment