WALIODAI KUPOTEZA KIMIUJIZA SEHEMU ZAO ZA SIRI SHINYANGA WASHIKILIWA NA POLISI

 

Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga linawashikilia watu wawili wakazi wa Wilaya ya Kahama, kwa tuhuma za kutoa taarifa za uongo na kuzua taharuki kwa madai ya kupoteza kimiujiza sehemu zao za siri.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, SACP Janeth Magomi, amesema tukio la kwanza limetokea Aprili 4, 2026 katika eneo la soko kuu mjini Kahama, ambapo Kisaka Elinihaki (22) alidai kupoteza sehemu zake za siri baada ya kushikwa bega la kushoto na Joseph Godfrey (36).

Tukio hilo lilisababisha wananchi kujaribu kumshambulia Godfrey kabla ya kuokolewa na polisi.

Amesema tukio la pili lilitokea Aprili 6, 2026 katika eneo la machimbo ya dhahabu Mwime, Kahama, ambapo Makoye James alitoa madai kama hayo dhidi ya Hamis Kumalija ambaye walikuwa wakisafiri naye kwenye Pikipiki, hali iliyosababisha mkusanyiko wa wananchi waliotaka kujichukulia sheria mkononi, kabla ya kudhibitiwa na Polisi.

Kamanda Magomi amesema uchunguzi wa kitabibu umebaini kuwa madai ya watu hao si ya kweli, kwani hawakuwa na mapungufu yoyote  kwenye sehemu zao siri.

Amesema watuhumiwa hao wanashikiliwa kwa kutoa taarifa za uongo na kusababisha taharuki, na hatua za kisheria zinaendelea.

Aidha, ametoa wito kwa wananchi kuacha kusambaza taarifa za uongo na badala yake washirikiane na vyombo vya ulinzi na usalama ili kudumisha amani.

 

No comments

#tuandikie maoni yako.

Theme images by Storman. Powered by Blogger.