WIVU WA MAPENZI WAENDELEA KUGHARIMU MAISHA YA WANANDOA; POLISI YAMSAKA MSHUKIWA
Mwanamke
mmoja mkazi wa Kijiji cha Songambele, Kata ya Salawe katika Halmashauri ya
Wilaya ya Shinyanga, amefariki dunia kufuatia kile kinachodaiwa kuwa ni
shambulio kutoka kwa aliyekuwa mume wake, likihusishwa na wivu wa mapenzi.
Tukio hilo
limegundulika Jumatatu, Machi 23, 2026 majira ya saa moja asubuhi, ambapo
mwanamke huyo aitwaye Mariam Cosmasi Mafumba (40), alikutwa amefariki dunia
ndani ya nyumba yake katika mazingira ya kutatanisha.
Kamanda wa
Polisi Mkoa wa Shinyanga, SACP Janeth Magomi, amethibitisha kutokea kwa tukio
hilo na kusema kuwa uchunguzi wa awali unaonyesha marehemu alipigwa kwa kitu
kigumu sehemu mbalimbali za mwili wake, ikiwemo kichwani, kabla ya kupoteza
maisha.
Ameeleza
kuwa chanzo cha tukio hilo kinahisiwa kuwa ni wivu wa kimapenzi, ambapo
mtuhumiwa alimshuku marehemu kuwa na mahusiano na wanaume wengine.
Kamanda
Magomi amelielezea tukio hilo kuwa ni la kikatili na kusema Jeshi la Polisi
linaendelea na uchunguzi, ikiwa ni pamoja na juhudi za kumtafuta mtuhumiwa
aliyetajwa kwa jina la Manyanda Mbuye, anayedaiwa kuwa mume wa marehemu.
Awali,
Mwenyekiti wa Kijiji cha Songambele, Lazaro Enock, alieleza kuwa kabla ya kifo
chake, Mariam alikuwa na mgogoro wa kifamilia na mume wake, uliyekuwa
akimtuhumu kuishi na mwanaume mwingine aliyemtambulisha kama ndugu yake, ingawa
baadaye ilibainika kuwa walikuwa na uhusiano wa kimapenzi.
Kwa mujibu
wa mwenyekiti huyo, watoto wa marehemu walidai kuwa mwanaume huyo ambaye
alikuwa ameondoka na kubeba vitu vyake, siku ya tukio alifika nyumbani usiku na
kuwataka waende kulala mapema na walipoamka asubuhi, walimkuta mama yao akiwa
amefariki dunia.

Post a Comment