WALIODAI KUPOTEZA KIMIUJIZA SEHEMU ZA SIRI WAHUKUMIWA KIFUNGO GEREZANI

 

Mahakama ya Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga imewahukumu kifungo cha gerezani watu wawili, wakazi wa Manispaa ya Kahama, baada ya kupatikana na hatia ya kutoa taarifa za uongo na kuzua taharuki.

Waliohukumiwa ni Kisaka Elinihaki (22), mfanyabiashara, aliyehukumiwa kifungo cha miezi sita gerezani, pamoja na Makoye James (20), dereva, aliyehukumiwa kifungo cha miezi mitano gerezani.

Hukumu ya Kisaka Elinihaki ilitolewa jana, Jumatano Aprili 8, 2026, huku ile ya Makoye James ikitolewa leo Alhamisi Aprili 9, 2026.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, SACP Janeth Magomi, watu hao walitoa taarifa za uongo wakidai kupoteza kimiujiza sehemu zao za siri baada ya kushikwa mabegani, katika matukio mawili tofauti.

Kamanda Magomi amesema kuwa baada ya uchunguzi, Jeshi la Polisi liliwakamata watuhumiwa hao na kuwafikisha mahakamani, ambapo walipatikana na hatia.

Aidha, amewataka wananchi kuacha tabia ya kutoa taarifa za uongo zinazoweza kusababisha taharuki, akisisitiza kuwa ni kosa la jinai. Ameongeza kuwa ni muhimu wananchi kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kudumisha ulinzi, usalama na amani.
 
 

No comments

#tuandikie maoni yako.

Theme images by Storman. Powered by Blogger.