MAPADRI WAWILI AMBAO NI WANAHABARI WABOBEVU WACHAGULIWA KUONGOZA SIGNIS DUNIANI NA AFRIKA

Padri Profesa Walter Chikwendu Ihejirika (Mwenye Miwani) na 
Padri Fedele Mutabazi (Mwenye koti) wakiwa kwenye Picha ya pamoja

Kigali Rwanda:
Na ANATOLI Salawa.

Mapadri wawili ambao ni wanahabari wambobevu wamechaguliwa kushika nafasi za juu za uongozi wa SIGNIS, shirika la kimataifa linalosimamia masuala ya habari na mawasiliano katika Kanisa Katoliki ulimwenguni.

Uchaguzi huo umefanyika wakati wa kilele cha Kongamano la Kimataifa la SIGNIS lililoanza Agosti 3, 2026, na kuhitimishwa mwishoni mwa wiki jijini Kigali, Rwanda, likiwakutanisha zaidi ya wanahabari 260 kutoka sehemu mbalimbali duniani.

Waliochaguliwa ni Padri Profesa Walter Chikwendu Ihejirika kutoka Nigeria, ambaye amechaguliwa kuwa Rais wa SIGNIS Ulimwenguni, huku Padri Fedele Mutabazi kutoka Rwanda akichaguliwa kuwa Rais wa SIGNIS Barani Afrika.

Kabla ya kuchaguliwa kuongoza SIGNIS Ulimwenguni, Profesa Ihejirika alikuwa Rais wa SIGNIS Barani Afrika, nafasi ambayo aliitumikia kwa ufanisi mkubwa akitumia uzoefu wake katika tasnia ya habari na mawasiliano.

Profesa Ihejirika pia alikuwa miongoni mwa viongozi walioshiriki kikamilifu katika maandalizi ya Kongamano la Kimataifa la SIGNIS lililofanyika jijini Kigali, ambalo lilihitimishwa kwa mafanikio makubwa baada ya washiriki kujadili kwa kina nafasi ya vyombo vya habari na mawasiliano katika kueneza ujumbe wa Kanisa, kuimarisha maadili ya uandishi wa habari na kutumia fursa za maendeleo ya teknolojia kuwafikia watu ili kujenga umoja, amani na mshikamano katika jamii.

Kwa upande wake, Padri Fedele Mutabazi alikuwa Katibu Mtendaji wa Tume ya Upashanaji Habari katika Baraza la Maaskofu Katoliki nchini Rwanda kabla ya kuchaguliwa kuwa Rais wa SIGNIS Barani Afrika.

Kuchaguliwa kwa viongozi hao kunatarajiwa kuimarisha nafasi ya SIGNIS katika kuendeleza matumizi ya habari na mawasiliano kama nyenzo muhimu ya uinjilishaji, elimu, mawasiliano na kujenga jamii yenye mshikamano.


Tanbihi: ANATOLI SALAWA ni Padri wa Jimbo Katoliki Shinyanga na Mkurugenzi wa Jimbo wa Idara ya Mawasiliano

No comments

#tuandikie maoni yako.

Theme images by Storman. Powered by Blogger.