RAFIKI SDO YAADHIMISHA SIKU YA MTOTO WA AFRIKA KWA MJADALA, WATOTO WATOA USHAURI KWA WZAZI NA JAMII
Shirika la kutetea haki za vijana, wanawake, watoto na watu wenye mahitaji maalum la RAFIKI SDO, leo jumanne tarehe 16, Juni, 2026, limeadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika kwa kuandaa mjadala maalum uliowakutanisha watoto na wadau mbalimbali kujadili haki, ustawi na maendeleo ya watoto.
Mjadala huo uliofanyika katika makao makuu ya shirika hilo yaliyopo Kata ya Kitangili, Manispaa ya Shinyanga, ambao uliongozwa na Mwenyekiti wa Baraza la Watoto Manispaa ya Shinyanga, Noelina Nicolaus Busisi.
Watoto walioshiriki
mjadala huo walisisitiza umuhimu wa malezi bora, mazingira salama na fursa sawa
kwa watoto wa kike na wa kiume.
Watoto hao pia
waliomba kuimarishwa kwa elimu ya afya ya uzazi ili kuwasaidia kujitambua na
kujikinga dhidi ya changamoto mbalimbali zinazotokana na kutokuwa na elimu
hiyo, ambazo ni pamoja na mimba za
utotoni, ndoa za mapema na maambukizi ya magonjwa ya zinaa.
Aidha, watoto
walieleza wasiwasi wao kuhusu matumizi yasiyodhibitiwa ya simu za mkononi na
vifaa vingine vya kielektroniki, wakitaka wazazi na walezi kuongeza usimamizi
ili kuwalinda dhidi ya athari za matumizi mabaya ya teknolojia.
Mbali na maoni hayo
ya watoto, washiriki wote wa mjadala huo walijadili changamoto ya watoto
wanaoishi katika mazingira hatarishi na hasa katika Kata ya Kitangili, ambapo
waliweka mikakati mbalimbali ya
kukabiliana na hali hiyo.
Baadhi ya mikakati
iliyopendekezwa ni pamoja na kuendelea kutoa elimu kwa jamii kupitia mikutano,
semina na kampeni za uhamasishaji kuhusu malezi bora na ulinzi wa watoto,
pamoja na kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali, wazazi, viongozi wa jamii na
wadau wa maendeleo katika kubaini mapema na kushughulikia changamoto zinazowakabili
watoto hao.
Akifungua mjadala
huo, Mkurugenzi wa RAFIKI SDO, Gerald Ng’ong’a, alipongeza juhudi za Serikali
katika kulinda haki za watoto kupitia utekelezaji wa sera mbalimbali, ikiwemo
sera ya elimu bila malipo na uanzishwaji wa mabaraza ya watoto yanayowapa
nafasi ya kusikika na kutetea haki za wenzao.
Alisema RAFIKI SDO
itaendelea kushirikiana na Serikali na wadau wengine katika kutoa elimu kwa
jamii, kuokoa watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi na kuhakikisha wazazi
na walezi wanatekeleza wajibu wao wa malezi.
Akihitimisha mjadala
huo, Diwani wa Viti Maalum katika Manispaa ya Shinyanga, Moshi Kanje, aliwataka
wadau wote kutekeleza mapendekezo yaliyotolewa na watoto ili kuhakikisha
wanakua katika mazingira salama na yanayowawezesha kufikia ndoto zao.
Siku ya Mtoto wa Afrika huadhimishwa kila mwaka Juni 16 kwa lengo la kuwakumbuka watoto wa Soweto nchini Afrika Kusini waliouawa na kujeruhiwa mwaka 1976 walipokuwa wakidai haki ya kupata elimu bora. Maadhimisho hayo yanalenga kuhamasisha jamii, serikali na wadau mbalimbali kuendelea kulinda na kutetea haki za watoto barani Afrika
Post a Comment